BARUA ZATOLEWA RASMI,WAPEWA SIKU 14
BAADA YA MAJIBU,KUJIELEZA KAMATI KUU
LISSU ADAI UTETEZI WAO ULIPOTOSHA UKWELI
Na Goodluck Hongo
Aliyekuwa
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Zitto
Kabwe pamoja na wenzake, wameandaliwa mashtaka 11 kwa madai ya kuandaa
mapinduzi ya siri dhidi ya uongozi wa chama hicho kinyume cha katiba.
Bw. Kabwe na wenzake ambao ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama
hicho, Dkt. Kitila Mkumbo na Bw. Samson Mwigamba, aliyekuwa Mwenyekiti wa
CHADEMA jijini Arusha, jana walikabidhiwa barua rasmi ili wajieleze ndani ya
siku 14.
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA, Bw. John Mnyika,
aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari
Makao Makuu ya chama hicho.
Bw.
Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ubungo, Dar es Salaam, alisema chama
hicho kimeandaa mashtaka hayo baada ya Sekretarieti ya CHADEMA kupitia maamuzi
ya Kamati Kuu yaliyowavua nyadhifa za uongozi watuhumiwa hao.
"Watuhumiwa
hawa watatakiwa kujieleza kwa maandishi ndani ya siku 14, baadaye watajieleza
mbele ya Kamati Kuu ambayo itatoa maamuzi ya hatua za kuchukua," alisema
Bw. Mnyika.
Alisema mashtaka hayo yametokana na waraka wa siri ambao
ulikamatwa na kutolewa mbele ya Kamati Kuu unaowakashifu viongozi wakuu wa
chama hicho.
"Wote watatakiwa kujieleza kwa nini wasifukuzwe ndani
ya chama chetu kwa makosa waliyofanya... Kamati Kuu ya chama ndicho chombo
chenye maamuzi ya kuwaondoa viongozi au wanachama wanaokiuka Katiba.
"Waraka uliochapishwa katika baadhi ya vyombo vya
habari (si Majira) na mitandao ya kijamii unaodaiwa kuwaponza Bw. Kabwe na
wenzake si wenyewe ni batili," alisema.
Aliongeza kuwa, maamuzi yaliyofanywa na Kamati Kuu
yalizingatia kanuni, sheria na taratibu za chama kwa kufuata katiba, hivyo Bw.
Kabwe na wenzake hawakufukuzwa kwa sababu walizozitoa kwenye vyombo vya habari
bali kwa kuandika waraka wa kimapinduzi.
Msimamo wa CHADEMA
Bw. Mnyika alisema, chama hicho hakipo tayari kuwavumilia
viongozi na wanachama wote ambao watakuwa kikwazo kwa chama hicho kufikia
malengo yake bila kujali cheo alichonacho.
"Wanatafuta huruma kwa wananchi kutokana na makosa
ambayo wameyafanya hasa la kuandaa waraka wa siri, wao wenyewe walikiri
kuhusika nao lakini wanapotosha ukweli," alisema.
Alisema Sekretarieti hiyo imepokea na kutoa mapendekezo
mbalimbali ya utekelezaji wa mikakati waliyojipangia ambayo ni Vuguvugu la
Mabadiliko (M4C) na "CHADEMA ni msingi".
Akizungumzia uchomaji wa bendera za chama, ofisi, fulana na
kuondoa mabango ya CHADEMA, baada ya Bw. Kabwe na wenzake kuvuliwa nyadhifa za
uongozi, Bw. Mnyika alisema chama kimezisikia taarifa hizo.
"Uchunguzi wa awali unaonesha kilichotokea ni kiini
macho tu si wanachama wa chama chetu waliofanya hivyo, viongozi wa maeneo
husika wanaendelea na vikao, usalama upo," alisema.
Tundu Lissu azungumza
Kwa upande wake, Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Bw. Tundu
Lissu, alisema watuhumiwa walifanya mkutano na vyombo vya habari kwa lengo la
kupotosha ukweli wa mambo juu ya mazingira halisi ya kuvuliwa nyadhifa zao.
"Hawakuondolewa katika nyadhifa zao kwa sababu ya kuuza
majimbo yetu ya uchaguzi mwaka 2010, si posho, wala uwepo wake kama Mwenyekiti
wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), aliyeibua hoja ya
kukaguliwa kwa hesabu za vyama vya siasa.
"Amevuliwa nyadhifa hizo na wenzake kwa sababu ya kuandaa
mapinduzi ndani ya chama kwa kukiuka maadili," alisema.
Akizungumzia madai ya kugawanyika au kupasuka kwa chama hicho kama
Bw. Kabwe atafukuzwa uanacham, Bw. Lissu alisema kwa nyaraka alizoziona, Kabwe
alikuwepo katika kikao cha Kamati Kuu kilichomfukuza aliyekuwa Katibu Mkuu wa
chama hicho mwaka 2004, Dkt. Amaan Kabourou.
"Ka bwe p i a a l i k uwe p o kwenye kikao cha Kamati Kuu
kilichomfukuza aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa chama hiki, marehemu Chacha
Wangwe mwaka 2007; hivyo hata kikao kama hicho ndicho kilichowavua vyeo yeye na
wenzie hivyo Kamati Kuu isilaumiwe," alisema.
Bw. Lissu alisema, madai ya Bw. Kabwe kudai alijitoa katika utiaji
saini katika masuala ya fedha ndani ya chama hicho kwanza hakuwahi kuwa mtiaji
saini ili kuidhinisha fedha, hivyo anashangaa kulizungumzia hilo wakati
hakuwahi kuwa mtiaji saini.
"Chama kimepasuka mara nyingi tangu enzi ya Bw. Kabwe kuingia
kwenye Kamati ya Jaji Bomani, Chacha Wangwe, ugaidi wa Rwakatare hata sakata la
mabomu lakini tuliibuka upya, hadi sasa chama kinaendelea na mapambano
yake," alisema.
Alipoulizwa na waandishi kama viongozi hao wakiamua kuondoka,
chama kimejipangaje, alisema si vizuri kuwahukumu Bw. Kabwe na wenzake kwa
sababu bado hawajaanza kujitetea, lakini kugombea uongozi ndani ya chama si
uhaini wala dhambi.
Alibainisha kuwa, sh. milioni 100 zilizotolewa na mfanyabiashara
maarufu nchini, Bw. Mustafa Sabodo, hesabu za matumizi yake zipo wazi na
zilipelekwa kwenye hesabu za chama hicho ili zikaguliwe na Mkaguzi na Mdhibiti
Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Aliongeza kuwa, licha ya vyama vya siasa kuwa tayari kukaguliwa,
CAG alishindwa kukagua hesabu hizo kwa sababu ya ukosefu wa fedha, hivyo
alivitaka vyama husika kuwalipa wakaguzi ambao wangefanya ukaguzi huo jambo
ambalo walilipinga.
"Tuna
ushahidi wote kuhusu suala hili, hata Msajili mpya wa Vyama vya Siasa,
aliandika barua kwa CAG kuhusu kupinga vyama kuwalipa wakaguzi wa hesabu kwani huo si utarabu wa Serikali, lakini
tunamshangaa Kabwe kuzungumzia suala hili wakati analijua vizuri," alisema
Bw. Lissu
No comments:
Post a Comment